Göttinger Predigten

Choose your language:
deutsch English español
português dansk

Startseite

Aktuelle Predigten

Archiv

Besondere Gelegenheiten

Suche

Links

Konzeption

Unsere Autoren weltweit

Kontakt
ISSN 2195-3171





Göttinger Predigten im Internet hg. von U. Nembach

KKKT DAYOSISI YA KASKAZINI, 11.03.2007

Predigt zu Exodus 1:15-22, verfasst von Peter E. Mremi

"Kisha mfalme wa Misri akasema na wazalisha wa Waebrania, mmoja jina lake aliitwa Shifra, na wa pili jina lake aliiitwa Pua; Akasema, wakati mwazalishapo wanawake kwa Kiebrania na kuwaona wa katika kuzaa, ikiwa ni mtoto mwanaume, basi mwueni, bali ikiwa ni mtoto mwanamke, na aishi. Lakini wale wazalisha walikuwa wakimcha Mungu, wasifanye kama walivyoamriwa na huyo mfalme wa Misri, lakini wakawahifadhi hai wale wanaume. Basi mfalme wa Misri akawaita wale wazalisha na kuwauliza, Kwa nini kufanya jambo hili, na kuwaifadhi watoto wanaume wawe hai? Wazalisha wakamwambia Farao, Ni kwa sababu hao wanawake wa Kiebrania si kama wanawake wa Kimisri kwa kuwa ni hodari nao, nao huzaa kabla mzalisha hajapata kuwafikilia. Basi Mungu akawatendea mema wale wazalisha; na hao watu wakaogezeka sana, wakaendelea na kuzidi kuwa na nguvu nyingi. Ilikuwa kwa sababu wale wazalisha walikuwa wakimcha Mungu, akawasimamishia nyumba. Kisha huyo Farao akawaagiza watu wake, akisema kila mtoto mwanaume atakayezaliwa mtatupa mtoni, na kila mtoto mwanamke mtamhifadhi hai" (Kut. 1:15 - 22).

 

Ninapotazama kichanga katika miguu ya mama yake najifunza mambo mengi. Naona upendo wa mama mwema ambaye hataruhusu wala sisimizi asiye na madhara kutambaa karibu na mtoto. Tena naona mtoto anayemtegemea mama kwa mambo yote. Mtoto hajui kama kuna hatari au kutindikiwa au lisilowezekana ali mradi tu mama yupo.

 

Mama na mtoto wanatazamana uso kwa furaha, kicheko na tabasamu, lakini si wakati wote. Kuna wakati mama anamwacha mtoto ili afanye mengineyo muhimu. Kuna wakati mtoto atasikia njaa na atalia sana. Kuna wakati mtoto atakwenda haja (choo) n.k. Kwa hiyo mambo mengi yataingilia kati ile hali ya furaha, kicheko, tabasamu na kutazamana nyuso.

 

Tunaweza kusoma hali kama hii kwa taifa teule la Mungu. Kuna wakati Mungu alipowashika mikono na kutazamana nao kwa upendo wenye matumaini makubwa, lakini pia Israel aliona njaa mpaka akajikuta yuko Misri, ila Mungu aliye mwaminifu ameendelea kumtunza Israel vizuri asiache hata sisimizi kutambaa juu ya mtoto huyu mpendwa.

 

 

MUNGU WETU HUWATETEA WANYONGE

 

Ulimwengu umeshuhudia wimbi kubwa la wakimbizi. Njaa, vita, uadui, wivu na hasira vimesababisha watu kuhama makwao kwenda kutafuta hifadhi mbali. Inawezekana pia wapo wanaokimbizwa na maovu yao ambao si shabaha ya neno letu la leo.

 

Watu wa Israeli walikuwa wakimbizi Misri baada ya kukimbia njaa nchini mwao. Lakini je, ukimbizi unaishia wapi? Mbona miaka ikawa mingi na vizazi vikapita? Kwa mpango wa Mungu Israel alipokelewa Misri kwa heshima kubwa kwa sababu alionekana kuwa Mwokozi kwa nchi ya Misri wakati ule alipokuwa familia chache tu. Lakini sivyo itakavyokuwa atakapoanza kuwa taifa.

 

Imefahamika hata leo watu wamekimbia nchi zao wakapata mafanikio makubwa ugenini na hivi wakasahau kusudi kwao. Si hayo tu bali wakati mwingine wameridhisha watoto na wajukuu zao chuki na uadui ambao pengine haupo. Ni vizuri kufahamu mpango wa Mungu katika hali na maisha hata yale ya ukimbizi. Je, Israeli alikuwa amesahau Ahadi ya Mungu ya urithi wa baba yao Abrahamu?

 

Inawezekana wakati wa mafanikio makubwa ugenini alisahau lakini Mungu alikuwa hajasahau agano lake. " Nitakufanya kuwa taifa kubwa ...(Mwa. 12:2)". Israeli kule Misri anaongezeka kwa haraka kuliko mwenyeji wake. Hata rafiki wa Israeli kama akina Pua na Shifra Mungu anawabariki. Swali la kujiuliza ni je, yawezekana kuwa taifa kubwa lifanyike ndani ya taifa jingine kubwa? Tunapaswa kukaa chini na kufikiri sana ni nini mapenzi na mpango wa Mungu.

 

Ametokea Farao ambaye hamjui Yusufu, ingawaje huyu ni mjinga sana kwa sababu anajua mipango maalumu iliyowekwa na Yusufu ya kuhifadhi vyakula kwa ajili ya kuinusuru nchi kutokana na njaa, kwa hiyo anatunga sera mpya za kupunguza kasi ya kuongezeka kwa wana wa Israeli lakini kwa kuipatia nchi faida kubwa ya miji ya kuhifadhia vyakula. Lakini mbinu ya Farao haikuwapunguza bali iliwaongeza kwa idadi, nguvu na maarifa, baraka ambayo Mungu ameshawaandalia.

 

Mpinzani wa mipango ya Mungu huanza hatua moja hadi nyingine. Ndogo na nyepesi lakini iliyojaa hila na asipofanikiwa kusonga mbele na majaribu mengine ya hatari zaidi. Tusiogope kujaribiwa lakini tujifunze kuangalia ule mlango wa kuondoka toka jaribu hilo uko wapi? 1 Kor. 10:13. Tumefikia mahali ambapo Israeli taifa dogo liko kwenye hatari ya kuangamia ndani ya taifa kubwa lenye wivu. Mtoto wa mama mzuri yuko kwenye hatari ya kunyemelewa na wadudu walio hatari. Mtoto anaogopa, analia lakini mama pia anaona. Mungu hamwachi mteule wake matesoni 2Pet. 2:9.

 

Farao anakubali maelezo dhaifu ya wakunga wa Waisraeli. Pengine huo ni mpango wa Mungu kwa sababu hoja ya wazalisha wale ingekuwa rahisi sana kujaribiwa. Lakini pia inawezekana amri potofu na katili ya Farao haikuwavutia raia wale. Kwa hiyo anaingia kwenye kosa la kutoa amri mbovu zaidi ya wazazi kuwa na watoto wao wenyewe.

 

Uongozi usiomtegemea Mungu licha ya kuwa hauna utii, lakini haufanikiwa katika malengo yake kwa sababu hekima ya kweli inatoka kwa Mungu.

 

 

MUNGU YUKO NA ISRAELI YA LEO KAMA ALIVYOKUWA NA TAIFA TEULE

Kanisa la Mungu ulimwenguni linapitia katika vipindi mbalimbali kama mtoto mchanga Kanisa la kweli linamtegemea Mungu kabisa. Wanaweza wakawapa Mafarao wanaolitesa Kanisa hapa ukimbizini (Ebr. 13:14) lakini nia ya Mungu kwa vyovyote hatimaye itashinda. Tujifunze kupokea maonyo ili tuhakikishe hatupambani na Mungu anapoliongoza na kulitunza Kanisa lake. Ikiwa Mungu ameweka mikononi mwetu jukumu la kuongoza watu wengine kama serikali au watunzaji wengine au jukumu la kuwahudumia wenzetu kiroho kwa Neno na Sakramenti siku zote tukumbuke kuwa Mungu ndiye kiongozi mkuu juu yetu. Tutapotumia vibaya madaraka au wajibu Mungu aliotupa Yeye mwenyewe atasimama kinyume na sisi na jambo hili ni hatari.

 

Kwa upande wa pili tusiogope wala kukata tamaa tunapojihisi kuonewa au kudhulumiwa. Tujue kuwa sisi si peke yetu. Yupo anayetuchunga vizuri na hatimaye atatupa kwa kadiri ya wingi wa utajiri wake, furaha tunayoitumainia.



Mch. Peter E. Mremi
Chuo cha Biblia na Theologia Mwika,
S.L.P 3050,
MOSHI

E-Mail: mwika@elct.org

(zurück zum Seitenanfang)